KIJANA
Haruni Kayombo (19), mkazi wa Mbalizi, Mbeya anaishi kwa mateso makubwa
tangu mwaka 2006, baada kushikwa na ugonjwa wa ajabu uliomuanza ghafla.
Katika
mahojiano na gazeti hili akiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)
jijini Dar es Salaam, Kayombo alisema bado hajui hatima ya maisha yake
kutokana na mateso anayoyapata usiku na mchana huku akitoa simulizi ya
majonzi namna gonjwa hilo lilivyomtokea.
Alisema
awali akiwa na umri wa miaka 11 alilazwa Hospitali ya Rufaa ya Mbeya
lakini baadaye wazazi wake walifariki dunia na hakupata kuwajua ndugu
zake jambo ambalo anaona hakuna haja ya kuwa binadamu huku akionekana
mwenye mateso makubwa.
“Sioni
faida ya kuwa binadamu, niliugua kama utani, ilifika wakati nikajua
kitu cha kawaida, nilishangaa kuona linazidi kuongezeka nilijua utakuwa
ugonjwa wa muda mfupi, lakini nikashangaa usiku na mchana mateso
yanazidi.
“Ni
tatizo ambalo hata mimi mwenyewe sijui chanzo chake, lilianza kama
kauvimbe ka kawaida, sikutambua mapema na sikuwa na hela kwenda kwenye
kituo cha afya kwa matibabu zaidi.
“Nilijipa
moyo kuwa ipo siku nitakuwa sawa lakini kwa mpaka sasa nimeshakata
tamaa, sina baba wala mama, hapa kweli kuna haja ya mimi kuitwa
binadamu? Sina kazi na sikubahatika kusoma ni nani atakayeokoa maisha
yangu?
“Maisha
haya ni Mungu tu anayeweza kuniokoa, inaniuma sana! Ningekuwa na ndugu
wangeweza kunisaidia japo hata pesa ya matumizi. Eee... Mola okoa maisha
yangu (analia). Napenda kuishi kama binadamu wengine lakini kwa hali
hii sina amani kabisa.
“Zamani
wakati tatizo linaanza nilikuwa na tabia ya kusali mara kwa mara lakini
nimefika hatua ya kukata tamaa na kuona hakuna haja.
“Namuomba
rais aje anitembelee ajionee mateso ninayoyapata usiku na mchana,
nimepangiwa kwenda kufanyiwa operesheni India lakini sijui lini na
itakuwaje!” alisimua Kayombo na kumaliza na kilio tena.
Kama
utakuwa umeguswa na tatizo la Haruni Kayombo basi usisite kutoa mchango
wako kwenye namba yake ya simu, mtumie kwa njia ya M-PESA ama wasiliana
naye moja kwa moja akiwa ndani ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa
namba +255764548607
No comments:
Post a Comment